Na Jacquiline Mrisho - MAELEZO. Waandishi wa Habari nchini wametakiwa kufanya utafiti wa taarifa wanazozitengeneza kabla hawajazitoa kwa jamii kupitia vyombo vya habari. Mkurugenzi wa Idara ya Habari-MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Hassan Abbasi ametoa rai hiyo leo jijini Dar es Salaam alipokuwa akifunga mafunzo ya Waandishi wa Habari za maendeleo yaliyotolewa na Wakfu wa Tasnia ya Habari Tanzania (TMF) juu ya usalama barabarani pamoja na masuala ya maendeleo. Dkt. Abbasi amesema kuwa Waandishi wa Habari wanatakiwa kufahamu haki na wajibu wa taaluma hiyo ambapo moja wapo ya wajibu wa mwanahabari ni kufanya utafiti wa chanzo na habari husika kabla ya kuifikisha kwa jamii ikiwa ni njia itakayosaidia kuzuia utoaji wa habari zisizo na uhakika kwa jamii. "Kutoa taarifa za uhakika kwa jamii kunahitaji taaluma na weledi wa hali ya juu, hivyo Wanahabari wanatakiwa wajikite zaidi katika kutafuta taarifa sahihi na kusisambaza kwa wananchi. Nawapongeza sana TMF pamoja na wadau wote walioshiriki katika uandaaji wa mafunzo haya." amesema Dkt. Abbasi. Dkt. Abbasi amefafanua kuwa Waandishi wa Habari wana haki ya kuikosoa Serikali ambapo Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016 katika kifungu cha 52 (2) imebainisha suaka hilo lakini taaluma, weledi haki na wajibu katika uandishi wa habari lazima vifuatwe. Amewaomba wafadhili wa mafunzo hayo pamoja na wadau wengine kutochoka kuwasaidia wanahabari ili waweze kutimiza majukumu yao ya kutoa taarifa kikamilifu na kuendelea kuwa washirika wa maendeleo nchini. Kwa upande wake Mkurugenzi wa TMF, Fausta Msokwa amesema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo Waandishi wa Habari kuwa wabobezi katika kutoa taarifa za uhakika za masuala mbalimbali ya maendeleo. "Mafunzo hayo yameleta uhai endelevu katika tasnia ya habari na kuwafanya Waandishi wa Habari kutoa habari zenye tija hasa katika kuelezea changamoto zilizopo maeneo ya vijijini," amesema Mkurugenzi Fausta. Mafunzo hayo yaliyoanza mwezi Mei mwaka jana na kuhusisha waandishi wa habari 15, yamefanyika kwa ushirikiano wa Wakfu wa Tasnia ya Habari Tanzania, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto pamoja na baraza la usalama barabarani na kufadhiliwa na Shirika la Afya Duniani pamoja na Taasisi ya Bloomberg. CAPTIONS 1. Mkurugenzi wa Idara ya Habari - MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Hassan Abbasi (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na mmoja wa Waandishi wa Habari aliyefanya vizuri katika mafunzo hayo, Adelina Bosco wakati wa kufunga mafunzo ya Waandishi wa Habari yaliyotolewa na Wakfu wa Tasnia ya Habari Tanzania (TMF) juu ya usalama barabarani pamoja na masuala ya maendeleo.Ufungaji huo umefanyika leo jijini Dar es Salaam. 2. Mkurugenzi wa Idara ya Habari - MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Hassan Abbasi (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na mmoja wa Waandishi wa Habari aliyepata tuzo zijulikanazo kama 'simema zetu' kwa kuandaa makala bora za Televisheni,Anwaly Msechu wakati wa kufunga mafunzo ya Waandishi wa Habari yaliyotolewa na Wakfu wa Tasnia ya Habari Tanzania (TMF) juu ya usalama barabarani pamoja na masuala ya maendeleo.Ufungaji huo umefanyika leo jijini Dar es Salaam. 3. Mkurugenzi wa Idara ya Habari - MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Hassan Abbasi (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na wadau, washiriki na wakufunzi baada ya kufunga mafunzo ya Waandishi wa Habari yaliyotolewa na Wakfu wa Tasnia ya Habari Tanzania (TMF) juu ya usalama barabarani pamoja na masuala ya maendeleo.Ufungaji huo umefanyika leo jijini Dar es Salaam.




Comments