Dkt. Mwakyembe : Atoa Rai kwa Kampuni ya Multichoice Kushirikiana na Wizara ya Elimu Katika Kukuza Elimu ya Sanaa. Na Lorietha Laurence-WHUSM, Dodoma Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe.Dkt. Harrison Mwakyembe ametoa rai kwa Kampuni ya Multichoice nchini kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na vyuo vinavyotoa elimu ya sanaa ya filamu ili kuhakikisha wanabadilishana ujuzi na kuwa na miradi ya pamoja. Dkt. Mwakyembe ameyasema hayo jana Jijini Dodoma wakati akizindua mradi wa kampuni hiyo utakaowapa fursa ya kujiendeleza kitaaluma vijana wenye vipaji katika tasnia ya filamu kwa kupata ufadhili wa mafunzo kwa muda wa mwaka mmoja katika chuo cha sanaa Jijini Nairobi nchini Kenya. “Napenda kuwapongeza Multichoice kwa kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha wanaleta maendeleo, huu ni mwanzo mzuri wa kuboresha taaluma kwa vijana ambao asilimia kubwa wamejiajiri katika sekta ya sanaa ikiwemo filamu” Dkt. Mwakyembe Aidha,Dkt. Mwakyembe amewataka vijana mabao wanakidhi vigezo kuhakikisha wanachangamkia fursa hiyo adimu ili waweze kuongeza ujuzi na hivyo kuwa chachu ya maendeleo pale wanaporudi nyumbani kwa kuwafundisha wengine ili elimu hiyo kuwafikia vijana wengi zaidi. Alizidi kufafanua kuwa ili kuwa na maudhui mazuri yenye kuvutia, yanayokwenda na wakati huku yakizingatia tamaduni za nchi yetu, ni lazima tuwe na wataalamu wetu wenyewe wa kuzalisha kazi hizo za kisanii, kuanzia waigizaji, waandika hadithi, waandaaji na wazalishaji. Naye Mkurugenzi Mtendaji Multichoice Africa - Mashariki na Magharibi, Bw. Maharage Chande ameeleza kuwa Multichoice Afrika imeanzisha Multichoice Talent Factory inayolenga kuwapa vijana wenye vipaji fursa maalum ya kupata mafunzo katika sekta ya filamu. “Kwa kuanzia tutakua na vituo vitatu vya mafunzo kimoja Afrika Magharibi, kingine Afrika Masharika na Afrika Kusini, ambapo vinatarajiwa kuanza rasmi mnamo mwezi Oktoba mwaka huu huku mchakato wa kupata wanafunzi utaanza mwezi Juni mwaka huu” Bw. Chande Adha Bw. Chande alisisitiza kuwa, katika kuhakikisha wanafanikisha zoezi hilo kwa ufanisi watashirikiana kwa karibu na wadau wa tasnia ya filamu hapa nchini katika mchakato mzima wa kuweza kuwapata vijana watakaofuzu kujiunga na mafunzo hayo.




Comments